Wednesday 21 February 2018

FAIDA ZA KUSAMEHE

1. Kwanza kabisa, tunasamehe kwa sababu kusamehe ni amri na ni agizo la Mungu. binadamu ni watu ambao hawapendi kukubali kosa ni watu waliozoea kujitetea na kukataa kosa pale anapokosa. Kama tukikataa kutii tunakaidi agizo la Mungu hivyo tunapaswa kusameheana kwani muasisi wa msamaha ni Mungu mwenyewe na kama Mungu angehesabu maovu yetu nani angesimama? Anza leo kusamehe, hakuna aliye mkamilifu.
2. Tunasamehe ili tuweze kusamehewa na pia ili maombi yetu yaweze kupokelewa na Mwenyezi Mungu. Unapaswa kusamehe kwa faida yako mwenyewe siyo kwa faida ya mkosaji na mwachie Mungu apambane na watesi wako wala usilipe kisasi wewe mwekee mtesi wako kaa la moto kichwani limchome. Kumwekea kaa la moto kichwani ni kama kumtesa kisakikolojia wewe unamsamehe yeye, amini basi nafsi yake inaendelea kumtafuna.
3. Unasamehe ili uwe na Amani ya moyoni mwako. Unaposamehe unakuwa unapata amani ya moyo. Mtu ambaye anavumilia uchungu ulioumbika ndani ya moyo na hataki kuachilia fundo hilo lazima litamtesa na atakosa amani ya moyo. Atahangaika na huku uchungu ulioumbika ndani ya moyo ukiendelea kumtafuta.
4. Unasamehe ili uwe na furaha moyoni mwako. Kwa kweli ukiangalia watu wanaokataa kusameheana huwa hawana furaha kabisa katika mioyo yao. Kama unaishi katika mahusiano yoyote na mara nyingi huwa watu si wakamilifu basi msamaha ndio kiunganishi chenu ambao utarudisha uhusiano uliopotea au uliovunjika na kuleta uhusiano wa awali yaani uhusiano mpya.

5. Tunasamhe ili tuwe na afya njema. Uponyaji wa kweli unaanzia moyoni. Kama mtu anasamehe kutoka moyoni basi huo ni msamaha wa kweli na ni msamaha unaongozwa na huruma ya Mungu ndani yake. Watu hawataki kusamehe ndio maana wengine afya zao ni dhaifu. Uchungu ulioumbika ndani ya moyo unaendelaa kumtafuna. Usizeeke kabla ya wakati kwa ajili ya kutosamhe.
6. Kutosamhe kunakufanya ujikinai wewe mwenyewe. Unajiona wewe ni mtu ambaye hustahili kuwepo hapa duniani. Utajiona wewe hauna maana hapa duniani utakua unakaa peke yako peke yako. Huna furaha, amani, upendo. Maisha yako yanakuwa yamejaa sumu na majeraha moyoni ugonjwa umekuwa mkubwa na wewe hutaki kuupatia dawa ya kuuponya na dawa yake ni msamaha tu.
7. Kutokusamhe kunaongeza maadui katika maisha yako. Kuna faida kubwa sana ya kusamehe. Jaribu kuangalia katika maisha yako Yule anayesamehe na asiyesamehe nani anakuwa anaongeza maadui? Utaongeza maadui na utavunja uhusiano na watu hivyo utakua unaishi maisha ya umimi. Maisha ya binadamu ni maisha yenye uhusiano kama husamehi basi unajitengenezea duniani yako mwenyewe.
8. Kutosamhe kunaleta mapasuko wa kifamilia. Katika hali ya kawaida jaribu kuangalia katika jamii yako ni familia ngapi zimesambaratika kwasababu ya kutosameheana ? ni nyingi sana kwanza familia nyingi zina migogoro ya aina mbalimbali inayosababishwa na watu kulipiana visasi na kutosameheana na kuishi maisha ya chuki kama ya paka na panya. Kusamehe ni faida kwa kila familia bora inayotaka amani na furaha, mipasuko katika familia itaendela kuwepo kama watu wasiposameheana.
9. Kutosamhe kunaleta unyonge wa moyo yaani huzuni. Ukiwaangalia watu wengine unawaonea huruma wanaishi maisha ya huzuni wakati falsafa ya maisha ni furaha hapa duniani. Tunatafuta kila siku ili tuweze kuwa na furaha. Inuka leo na nenda kazike hilo jeneza la huzuni na kuwa huru na maisha yako. Huoni ni utumwa kuwabeba watu moyoni? Hujaja duniani kuteseka na maisha ni mafupi sana samehe na endelea na maisha yako.
10. Kutosamhe kunawafanya watu kukimbia makazi na ofisi zao. Kwa mfano, watu waliokoseana na hawataki kusameheana huwa wanaishi maisha kama ya paka na panya. Akimuona mwenzake huyo anakuja anakimbia kama yuko nyumbani anakimbia, kama ni njia anabadilisha kabisa ili wasionane na kusalimiana. Unakuta watu wengine wanakimbia kabisa ofisi zao kwa sababu ya kutotaka kusameheana. Kwanini uendelea kuishi maisha haya? Anza kubadilika kama ulikuwa unakimbia makazi au ofisi ili usikutane na mtesi wako.

Maisha ya kutokusamehe yanahasara nyingi na faida ni nyingi zaidi kuliko hasara. Imani za watu zinakufa kwa ajili ya kutokusamehe, watu wanazeeka mapema kabla ya muda, watoto wa mitaani wanaongezeka kwa ajili ya kutokusamehe yaani; pale wazazi wanapotalakiana na kuwatelekeza watoto. Tuishi katika maisha ya kusameheana na siyo ya kulipizana visasi.


Kwa ushauri tuwasiliane kwa barua-pepe fkmwamoto@gmail.com au Whatsapp 0784190882